SARATANI YA MATITI BADO NI TATIZO KWA WANAWAKE NA WASICHANA DUNIANI.
Na Siti Ali.
Saratani ya matiti ndiyo inayoongoza
duniani ambayo ni chanzo kikuu cha vifo vinavyohusiana na saratani kwa
wanawake.
Utambuzi wa mapema ni muhimu sana
ili kupata matokeo mazuri na kuongeza uwezekano wa kupona. Katika mwezi
wa Oktoba, ambao duniani kote unatambuliwa kama mwezi wa uhamasishaji dhidi ya
saratani ya matiti, Shirika la Afya Duniani (WHO) linaelekeza juhudi zake
katika kuongeza uelewa, kuhimiza uchunguzi wa mapema, na kuimarisha huduma za matibabu
na kinga. Kwa mujibu wa takwimu za kimataifa, inakadiriwa kuwa kila baada ya
dakika nne, mwanamke hugunduliwa na saratani ya matiti, jambo linaloonesha
uzito wa tatizo hili kiafya na kijamii.
Licha ya kuongezeka kwa ugonjwa
wa saratani ya matiti kwa wanawake, zipo jitihada mbalimbali zinazochukuliwa na
Serikali pamoja na wadau ili kupunguza kasi ya maambukizi na athari zake.
Jitihada hizo zinajumuisha utoaji wa elimu kuhusu ugonjwa huo, ikiwemo namna ya
kujichunguza mwenyewe hatua ambayo inawasaidia wanawake wengi nchini kutambua
dalili za awali.
Akizungumzia juhudi hizo, Daktari
Bingwa wa Magonjwa ya Jamii kutoka Asasi ya Jafaygo, Dkt. Merry Rose Kawajiata,
alisema kuwa wamekuwa wakishirikiana na Wizara ya Afya chini ya Serikali ya
Mapinduzi ya Zanzibar katika kutoa mafunzo kwa wahudumu wa afya ili kuwawezesha
kufanya uchunguzi wa saratani ya matiti kwa ufanisi.
“Tumekuwa tukishirikiana na
Wizara ya Afya kupitia Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kutoa mafunzo
kwa wahudumu wa afya ili waweze kufanya uchunguzi wa saratani ya matiti, pamoja
na kutoa matibabu ya awali mara tu ugonjwa huu unapogundulika,” alieleza Dkt.
Merry.
Hata hivyo, Dkt. Merry alisema
kuwa zaidi ya asilimia 50 ya wanawake hupoteza maisha kutokana na saratani ya
matiti, sambamba na kueleza viashiria vinavyochangia kupatikana kwa ugonjwa
huo, ikiwemo umri, urithi, uzito mkubwa, kutokunyonyesha, kutofanya mazoezi,
matumizi ya tumbaku, na kuchelewa kupata mtoto.
“Hakuna sababu moja maalumu inayosababisha saratani ya matiti, bali vichocheo vya hatari vinavyoweza kuchangia ni pamoja na kupata hedhi mapema kabla ya umri wa miaka 11, kuchelewa kukoma hedhi zaidi ya miaka 55, kuwa na historia ya saratani katika familia au kupata saratani kwa njia ya kurithi. Aidha, wanawake kutokunyonyesha au kunyonyesha kwa muda mfupi, kuwa na uzito mkubwa kupita kiasi, kupata mtoto baada ya miaka 35, pamoja na matumizi ya tumbaku au pombe, ni miongoni mwa sababu zinazoongeza hatari,” alifafanua Dkt. Merry.
Kwa upande wake, Afisa wa Maradhi
ya Saratani ya Matiti na Mlango wa Kizazi kutoka Wizara ya Afya, Kitengo
Shirikishi cha Mama na Mtoto, Mwanafatima Ali Mohammed, kwa ushirikiano na
Asasi ya Jafaygo kupitia ufadhili wa Faidha Foundation, alisema wamekuwa
wakitekeleza jitihada mbalimbali za utoaji elimu kwa jamii kwa kutembelea wilaya
na shehia mbali mbali ili kuwafikia wanawake wengi zaidi kwa ajili ya elimu na
uchunguzi wa saratani ya matiti.
Alisema kuwa takwimu za mwaka
jana zinaonesha kuwa mwezi Juni pekee, watu 7,400 waliweza kufanyiwa uchunguzi
wa saratani ya matiti Unguja na Pemba. Aidha, kuanzia Juni hadi Oktoba mwaka
huu, watu wasiopungua 3,000 tayari wamepimwa, na zoezi hilo linaendelea.
Mwanafatima alitoa wito kwa jamii
kuendelea kujenga utamaduni wa kutembelea vituo vya afya kwa ajili ya
kujichunguza, akisisitiza kuwa saratani ya matiti ikigundulika mapema
inatibika.
Subira Ali Hamza, mama wa watoto
watatu kutoka Matemwe na mmoja wa waliowahi kuathirika na saratani ya matiti,
alielezea namna alivyogundua ugonjwa huo na kupatiwa matibabu hadi kupona, huku
akitoa shukurani kwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kupitia Kitengo
Shirikishi cha Mama na Mtoto kwa huduma alizopata.
“Mimi nilianza kuhisi maumivu ya
ziwa nikaanza kutumia dawa za kienyeji, lakini siku moja nikasikia gari la
matangazo likitoa elimu kuhusu saratani ya matiti. Niliamua kuchukua hatua na
kufika hospitali, ambako nilipatiwa matibabu na kwa neema ya Mungu niliweza
kupona na sasa afya yangu imeimarika,” alisema Subira.
Alitoa wito kwa wanawake na
wasichana kutokukimbilia tiba zisizothibitishwa na badala yake kufika hospitali
mapema pindi wanapohisi mabadiliko yoyote, ili kupata uchunguzi na matibabu
sahihi.
jamii imesisitizwa kuchukua
tahadhari kwa kujenga utamaduni wa kuchunguza afya mara kwa mara, kuachana na
mila potofu zinazoathiri juhudi za matibabu, na kuhakikisha wanawahi kupata
huduma za hospitali kwa kuwa saratani ya matiti inatibika ikiwa itagundulika
mapema. Kinga ni bora kuliko tiba.


No comments