ZIDO YATOA MSAADA WA SHILINGI MILIONI 30 KWA WATU WENYE ULEMAVU .
Na Safia Mohammed.
Taasisi ya Zanzibar International Development Organization (ZIDO) imesema itaendelea na juhudi za kukuza na kuimarisha ustawi wa wananchi hasa watoto yatima na makundi ya watu wenye ulemavu nchini.
Mkurugenzi wa Taasisi hiyo Ramadhan Makame Mbanja ameseyasema hayo huko Dunga wakati akikabidhi vitu mbalimbali kwa watoto yatima, watu wenye ulamavu wa viungo pamoja na ngozi.
Amesema Taasisi hiyo imekuwa ikitoa msaada wa karibu kwa makundi hayo kwa kuyasaidia mahitaji na huduma mbalimbali ili kuhakikisha na wao wanajiona sawa na watu wengine katika jamii na wanastahili kupata haki zote za msingi.
Amesema vifaa hivyo vilivyogharimu jumla ya shilingi milioni thalathini vitawarahisishia katika shughuli zao za kiuchumi, kielimu na kimaisha.
Afisa ulemavu Wilaya ya Kati ndugu Abdalla Aladi amesema utolewaji wa vifaa hivyo kwa watu wa makundi ya watu wenye ulemavu unatoa faraja na furaha kwani huweza kutimiza ndoto zao za maisha.
Aidha amewahimiza wazazi wenye watoto wenye ulemavu kutowaficha majumbani na badala yake kwenda kuwaorodhesha wilayani ili waweze kutambulika na kupatiwa haki zao za msingi.
Katibu wa Taasisi ya watu wenye ualbino Zanzibar Mohd Ali Mohd na wananchi waliopatiwa msaada huo Mwanakombo Mohammed na bwana Ali Mzee wameelezea kufurahishwa kwao na misaada hiyo waliopatiwa kwani itawarahisishia shughuli zao ikiwemo za malezi pamoja na kujiwezesha kiuchumi.
No comments