TAMWA-ZNZ YAWAWEZESHA WAFANYAKAZI WA SEKTA ISIYO RASMI KUKABILIANA NA UKATILI WA KIJINSIA
Na Said khamis.
Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake Zanzibar (TAMWA-ZNZ) kimeandaa mafunzo maalum kwa viongozi na wafanyakazi wa sekta isiyo rasmi kutoka Wilaya ya Kaskazini A, Unguja, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kupambana na udhalilishaji na ukatili wa kijinsia katika jamii.
Mafunzo hayo yamewakutanisha
wadau mbalimbali wakiwemo wafanyakazi wa masokoni, mama ntilie, wanikaji wa
dagaa, wakulima wa mwani, wavunaji wa majongoo bahari, wavuvi, manahodha,
wafanyabiashara ndogo ndogo pamoja na wakulima wa muhogo na ndizi, kwa lengo la
kuwajengea uelewa na uwezo wa kukabiliana na changamoto zinazowakabili katika
maeneo yao ya kazi na maisha ya kila siku.
Akifungua mafunzo hayo, Mkuu
wa Maafisa Programu kutoka TAMWA-ZNZ, Zaina Abdalla Mzee, amesema kuwa
udhalilishaji na ukatili wa kijinsia dhidi ya wanawake na wasichana ni janga la
kidunia linalokiuka haki za binadamu, na kusisitiza kuwa kila mtu ana wajibu wa
kushiriki katika kupinga vitendo hivyo.
“Ni muhimu kwa kila mmoja
wetu kuchukua hatua za makusudi kuhakikisha tunajiepusha na kushiriki katika
vitendo vya udhalilishaji na ukatili, pamoja na kulinda haki za wanawake na
watoto,” amesema Zaina.
Kwa upande wake, Afisa
Programu wa TAMWA-ZNZ, Asia Hakim Makame, amesema kuwa mafunzo hayo yanalenga
kuwajengea washiriki uelewa kuhusu aina mbalimbali za ukatili wa kijinsia
unaoweza kutokea katika maeneo yao ya kazi, njia sahihi za kuripoti matukio
hayo, pamoja na kutambua haki zao kama wafanyakazi.
Ameongeza kuwa kupitia
mafunzo hayo, washiriki watawezeshwa kujenga mazingira salama na yenye usawa,
huku wakihamasishwa kushiriki kikamilifu katika kupinga vitendo vya ukatili
dhidi ya wanawake na wasichana katika jamii zao.
Mkufunzi wa mafunzo hayo,
ambaye pia ni mwanaharakati wa kupambana na ukatili wa kijinsia, Sabahi Bakar
Hassan, amesema kuwa vitendo vya udhalilishaji vinaweza kumtokea mtu yeyote
bila kujali jinsia au umri, lakini wanawake na wasichana wako katika hatari
zaidi kutokana na mila na desturi potofu zilizojengeka katika jamii.
Amesisitiza kuwa ukosefu wa
uwajibikaji katika mifumo ya utoaji haki huchangia kuendelea kwa vitendo hivyo,
na kutoa wito wa kuimarishwa kwa ushirikiano kati ya sekta mbalimbali na jamii
kwa ujumla ili kukabiliana na changamoto hiyo.
Washiriki wa mafunzo hayo
wameeleza dhamira yao ya kuwa mabalozi wa mabadiliko katika jamii, kwa
kuhakikisha wanapinga na kukemea vitendo vya ukatili wa kijinsia katika maeneo
yao ya kazi na makazi.
Mafunzo hayo ni sehemu ya
utekelezaji wa Mradi wa “Tunaweza Pamoja” unaotekelezwa na UN Women kwa
kushirikiana na TAMWA Zanzibar, kwa ufadhili wa Serikali ya Norway chini ya
mpango wa pamoja wa Umoja wa Mataifa, unaolenga kujenga jamii salama, yenye
usawa na isiyovumilia ukatili dhidi ya wanawake na wasichana.

No comments