Breaking News

TAMWA-ZNZ YAJA KIVYENGINE YAONGEZA NGUVU SEKTA YA USAFIRISHAJI, MAPAMBANO DHIDI YA UDHALILISHAJI WA KIJINSIA.

 


Na Fatma Rajab.

Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania Zanzibar (TAMWA-ZNZ) kimetoa mafunzo maalum ya siku moja kwa watoa huduma za usafirishaji wa umma kutoka Wilaya ya Kaskazini A, Unguja, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuimarisha mapambano dhidi ya udhalilishaji na ukatili wa kijinsia katika sekta ya usafirishaji visiwani Zanzibar.

Lengo la mafunzo hayo ni kuwajengea uelewa na kuwashirikisha watoa huduma wa usafiri usio rasmi katika kuzuia na kupambana na vitendo vya ukatili na udhalilishaji dhidi ya wanawake na watoto wa kike, pamoja na kuhakikisha wanawake na wasichana wanapata huduma za usafiri katika mazingira salama na yenye heshima.

Akizungumza katika mafunzo hayo yaliyofanyika katika Ukumbi wa Mkoa wa Kaskazini Unguja, Mkokotoni, Afisa Programu kutoka TAMWA-ZNZ, Asia Hakim Makame, amesema mafunzo hayo yataongeza uwajibikaji kwa watoa huduma za usafiri, kubadili mitazamo hasi kuhusu wanawake na kusaidia kuifanya sekta ya usafiri kuwa sehemu salama kwa wanawake wanaotumia usafiri huo na jamii.



Amesema kupitia mafunzo hayo, washiriki wameshirikishwa kuandaa na kukubaliana kwa pamoja Kanuni ya Maadili (Code of Conduct) itakayowaongoza katika utoaji wa huduma kwa kuzingatia misingi ya heshima, usalama na uwajibikaji.

“Kanuni hiyo inalenga kuhakikisha wanawake na wasichana wanaheshimiwa, kuzuia vitendo vya unyanyasaji wa kijinsia, matumizi ya lugha chafu na vitisho, kulinda usalama wa abiria wakati wa safari, pamoja na kuripoti matukio ya ukatili au udhalilishaji yatakayoshuhudiwa,” amesema Asia.

Aidha, amesema hatua hiyo itasaidia kujenga mazingira salama na rafiki kwa wanawake na watoto wa kike wanapotumia vyombo vya usafiri wa umma.

Kwa upande wake, mtoa mada kuhusu mabadiliko ya kitabia kutoka Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Zanzibar, Mohamed Jabir Makame, amesema baadhi ya vitendo vya udhalilishaji katika sekta ya usafiri husababishwa na ukosefu wa elimu kuhusu heshima, maadili na nidhamu kwa watoa huduma.



Amesema elimu hiyo itawasaidia watoa huduma kutambua vitendo vya ukatili wa kijinsia na kuepuka kuvifanya kwa makusudi au bila kutambua madhara yake kwa jamii.

Washiriki wa mafunzo hayo wameeleza kuwa changamoto ya udhalilishaji katika sekta ya usafiri ipo kwa pande zote mbili kati ya dereva na abiria, hivyo wamependekeza elimu hiyo kuendelea kutolewa kwa jamii nzima ili kuongeza uelewa na kujenga mahusiano yenye kuheshimiana.

Washiriki hao pia wameahidi kuwa mabalozi wa kupinga ukatili wa kijinsia na kulinda usalama wa wanawake na wasichana katika maeneo yao ya kazi na jamii kwa ujumla.

Mafunzo hayo yamewakutanisha wadau mbalimbali wakiwemo waendesha bodaboda, , madereva wa magari ya abiria, madereva wa bajaji, askari wa usalama barabarani pamoja na Afisa Takwimu kutoka Ofisi ya Mtakwimu Mkuu wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar.

 



Mafunzo hayo ni sehemu ya utekelezaji wa Mradi wa “Tunaweza Pamoja” unaotekelezwa na UN Women kwa kushirikiana na TAMWA Zanzibar kwa ufadhili wa Serikali ya Norway chini ya mpango wa pamoja wa Umoja wa Mataifa unaolenga kujenga jamii salama, yenye usawa na isiyovumilia ukatili dhidi ya wanawake na wasichana.



No comments