Breaking News

TAHADHARI ZA MAAMBUKIZI KWA VIJANA BADO ZINAHITAJIKA ILI KUMALIZA UKIMWI ZANZIBAR.



Na Siti Ali.

Licha ya serikali na wadau mbali mbali kutoa elimu juu ya maambukizi ya virusi vya ukimwi kwa njia tofauti lakini watu wengi hususani vijana wanapuuza tahadhari zinazotolewa na kujiingiza katika tabia hatarishi zinazosababisha kupata maambukizi ya vvu na ukimwi.

Ni vyema kila mtu aseme sasa basi kila ajikinge na maambukizi ya ukimwi kwani njia moja wapo ya kupata usalama ni kuepukana na tabia hatarishi,lakini sio vizuri kumdhania mtu kuwa ameambukizwa,pia si vyema kumuamini mtu kuwa yupo salama kwa kumuangalia kwa macho tu kwani macho kazi yake ni kuona.

Ifahamike kwamba kuona nje sura ya mtu na umbo lake lakini ni vizuri kuwa na tabia ya kujichunguza mara kwa mara ili kujua hali yako inavyoendelea hasa kwa kuangalia maambukizi ya vvu.

Inasikitika pia vijana wengi hujiingiza katika vitendo vya kujamiiana katika umri mdogo ambapo baadhi yao wapo skuli za msingi,sababu kuu ya zinazotajwa kwa vijana kujiingiza katika tabia hatarishi zinazopelekea  kuambukizwa virusi vinavyosababisha ukimwi ni pamoja na mazingira ya kisasa yaliyotawaliwa na utandawazi na kuwa mahodari wa kuiga maovu,kuwa na tamaa kushawishika na teknolojia na kuendekeza shindikizo rika.

Watu waliomo kwenye kundi hili ni wengi na wanaishi katika mazingira mchanganyiko miongoni mwao ni utashi,hamasa hisia na mihemko ya kimaumbile ambayo hujiingiza katika ngono na hatimae hupata vvu.

Kutokana na hali hii ipo haja ya kutolewa elimu na nasaha ya mapema kwa vijana ili wasubiri, kwani kila kitu kina wakati wake,imebainika kwamba kundi la vijana wenye umri wa miaka 9 hadi 24 ndio walio katika hatari Zaidi ya kuambukizwa vvu.

Jamii inatakiwa isisitize maadili mema na mila nzuri za kizanzibar ili kuepuka kufanya ngono katika umri mdogo,kwani watu watatu wa mwanzo wameambukizwa vvu hapa Zanzibar waligunduliwa mwaka 1986.



Tume ya ukimwi Zanzibar ZAC wamekuwa mstari wa mbele katika kuongoza mapambano dhidi ya maambukizo mapya ya vvu ili kutimiza lengo la kimataifa la kumaliza ukimwi ifikapo mwaka 2030.ZAC imeendelea kutoa wito wa mashirikiano ya pamoja kwa wadau wote na kukumbuka kwamba nguvu za pamoja katika kinga,tiba na huduma nyengine za ukimwi zitatufikisha kwenye lengo lililokusudiwa la kumaliza ukimwi duniani.

Akieleza hali ya maambukizi ya ukimwi Zanzibar Mwenyekiti wa bodi ya Tume ya UKIMWI Zanzibar Dr Ali Salim Ali amesema kuwa kwa mwaka wa 2025kupitia vituo vinavyotoa huduma za ushauri nasaha na uchunguzi wav vu,jumla ya watu 105,756walipimwa kati yao wanawake walikuwa 58,359 sawa na asilimia (55%)na wanaume ni 47,397sawa na asilimia (45%).

“Katika takwimu hizi watu 79,526 sawa na asilimia (75%)walipimwa Unguja na 26,230(25%)walipimwa Pemba .Jumla ya watu 697sawa na asilimia 0.7)waligundulika na maambukizi ya vvu ,kati ya hao wanawake ni 466 sawa na asilimia (67%)na wanaume ni 231 sawa na asilimia (33%)”ameeleza Dr Salim.

Aidha ameendelea kusema kuwa takwimu za maambukizi ya kwa umri zinaonesha kuwa kundi lenye maambukizo mengi Zaidi ni la umri wa miaka 25-49 ambalo linachangia asilimia 71% ya maambukizo yote yaliyorikodiwa likifuatiwa na kundi la umri wa miaka 20-24.Takwimu hizi zinaashiria uhitaji wa kuimarisha mikakati ya kinga na elimu ya vvu,pamoja na kuendelea kuelimisha vijana ili kupunguza tabia hatarishi walizonazo.

Sambamba na hayo amesema juhudi za kuzuia maambukizo ya vvu kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto zimeonesha mafanikio makubwa.Hadi kufikia septemba jumla ya wajawazito 53,706 walihudhuria klinik kati yao kinamama 53,031 walifanyiwa vipimo vya vvu,ikiwa ni sawa na asiimia 99%ya waliohudhuria kliniki.

“Miongoni mwa kinamama waliopimwa 89 walikutwa na maambukizi ya vvu ambao ni sawa na asilimia 0.2 ya wale waliopimwa.Kwa watoto waliozaliwa na mama wenye vvu ,jumla ya watoto 362 walipimwa kwa kutumia kipimo cha DNA-PCR,kati yao watoto wawili 2 waligundulika na vvu ambao ni sawa na asilimia 0.5% ya kiwango cha maambukizo.Mafanikio haya yanaonesha maendeleo chanya katika kufikia hatua ya kumaliza maambukizo ya vvu kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto”ameeleza Dr Ali.

 Akizungumza katika maadhimisho ya siku ya ukimwi duniani huko katika ukumbi wa sheikh Idrisa Abdulwakil kikwajuni makamo wa pili wa Zanzibar Mh Hemed Sueiman Abdulla amesema kuwa Zanzibar imefanikiwa kupunguza maambukizi mapya ya maradhi ya ukimwi kutoka watu 362 kwa mwaka 2020 hadi kufikia watu 211 waliopata maambukizi mapya ya kwa mwaka 2025 jambo lililosaidia kupunguza vifo vinavyotokana na maradhi ya ukimwi kutoka vifo 230 kwa mwaka 2020 hadi vifo 115kwa mwaka 2025.

Mh Hemed amefahamisha kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imeandaa mpango maalumu unaojulikana kwa jina la “Mpango endelevu wa kupambana na Ukimwi Zanzibar”wenye lengo la la kuhakikisha mapambano dhidi ya ukimwi yanakuwa endelevu ili kufikia lengo la kumaliza ukimwi ifikapo 2030.

Aidha Makamo wa pili wa rais amewahakikishia watu wanaoishi na virusi vya ukimwi kuwa serikali inayoongozwa na Dkt.Hussein Mwinyi itazifanyia kazi changamoto zilizowasilishwa na jumuiya ya watu wanaoishi na virusi vya ukimwi Zanzibar (ZAPHA+) ikiwemo kuongezwa bajeti kwa ajili ya upatikanaji wa dawa na vipimo kwa wagonjwa wa ukimwi,pia kuwezesha harakati za mapambano dhidi ya ugonjwa wa ukimwi nchini.

“Nawasihi wananchi kutowanyanyapaa na kuwabagua watu wanaoishi na virusi vya ukimwi kwani kufanya hivyo ni kurudisha nyuma jitihada za serikali za kumaliza maambukizi mapya ya ukimwi”amesema Mh Hemed.

Hata hivyo ametoa wito kwa taasisi wadau na jamii kwa ujumla kushirikiana na kwa pamoja katika kuhamasisha kampeni za mabadiliko ya tabia ,kuongeza ubunifu na upatikanaji wa fedha na vifaa ambavyo vikitumika kwa ufanisi lengo la kumaliza ukimwi Zanzibar litafikiwa.

“Natoa wito kwa taasisi wadau na jamii kwa ujumla kushirikiana na kwa pamoja katika kuhamasisha kampeni za mabadiliko ya tabia ,kuongeza ubunifu na upatikanaji wa fedha na vifaa ambavyo vikitumika kwa ufanisi lengo la kumaliza ukimwi Zanzibar litafikiwa ameeleza Mh Makamo.

Nao watu wanaoishi na virusi vya ukimwi Zanzibar kutoka jumuiya yya ZAPHA+ wamesema kuwa kutokana na mashirika na wafadhili kusuasua katika kutoa misaada hasa kwa watu wanaoishi na virusi vya ukimwi wameiombaserikali kuliangalia suala la dawa za ARV kuwekwa katika bajeti ya serikali ili huduma hiyo iendelee kwa wagonjwa wa ukimwi.

“Tunakabilwa na changamoto mbali mbali hii inatokana na mashirika na wafadhili kusuasua katika kutoa misaada hasa kwa watu wanaoishi na virusi vya ukimwi hivyo basi tunaiomba serikali kuliangalia suala la dawa za ARV na kuweka katika bajeti ya serikali ili huduma hiyo iendelee kwa wagonjwa wa ukimwi”wameeleza watu hao.

Aidha wamesema kuwa wagonjwa wa ukimwi wamekuwa wakikabiliwa na changamoto katika sehemu za utoaji wa huduma za kijamii hivyo wameiomba serikali kuwasaidiwa kutambulika kupitia katika mifumo mbali mbali ya utoaji wa huduma hasa hospitali ili waweze kupatiwa huduma ambazo zitapelekea kuwaondoshea usumbufu.

“Tunaiomba serikali kutusaidia kutambulika katika mifumo mbali mbali ya utoaji wa huduma hasa hospitali ili tuweze kupatiwa huduma ambazo zitapelekea kutuondoshea usumbufu”wamesema.

Sambamba na hayo wamesema kuwa katika kukabiliana na usumbufu dhidi ya ukimwi,hivyo basi serikali inapaswa kuanzisha mfumo maalumu mapambano dhidi ya ukimwi ambao utakabiliana na upungufu wa fedha kwa ajili ya upatikanaji wa huduma muhimu kwa watu wanaoishi na ugonjwa wa ukimwi  

Vile vile usiwaamini moja kwa moja wanaodai kuwa wamepimwa na kuonekana salama kwa kuwa ana cheti kwani kuwa na cheti sio usalama wa kudumu,inawezekana alopimwa jana au mwezi uliopita leo akagundulika na VVU,hivyo basi kila mmoja wetu anapaswa kuwa makini kwa kuwamua kwa makusudi kupima afya yake na kuachana na tabia zinazohatarisha maisha.

Jamii inatakiwa kuchukuwa tahadhari kubwa kwa ugonjwa huu ambao athari zake zinasikitisha sana kwa kuwepo unyanyapaa na kuongezeka watoto wanaoishikatika mazingira magumu kwani muda mrefu tumeshuhudia ndugu zetu wakipoteza maisha kutokana na ugonjwa huu,na tunaweza kusema kwamba hakuna familia ambayo haijaguswa na ugonjwa huu.

Hivyo basi kila mmoja achukuwe tahadhari juu ya ugonjwa huu kwani  kinga ni bora kuliko tiba.


No comments